Swahili New Testament Bible

Luke 11

Luke

Return to Index

Chapter 12

1


 

  Wakati watu kwa maelfu walipokuwa wamekusanyika hata wakawa wanakanyagana, Yesu aliwaambia kwanza wanafunzi wake, "Jihadharini na chachu ya Mafarisayo, yaani unafiki.  

 

 

-

2


 

  Kila kilichofunikwa kitafunuliwa, kila kilichofichika kitafichuliwa.  

 

 

-

3


 

  Kwa hiyo, kila mliyosema gizani, watu watayasikia katika mwanga, na kila mliyonong`ona faraghani milango imefungwa, yatatangazwa juu ya nyumba.  

 

 

-

4


 

  "Nawaambieni ninyi rafiki zangu: msiwaogope wale wanaoua mwili, wasiweze kufanya kitu kingine zaidi.  

 

 

-

5


 

  Nitawaonyesheni yule ambaye ni lazima kumwogopa: mwogopeni yule ambaye baada ya kuua ana uwezo wa kumtupa mtu katika moto wa Jehanamu. Naam, ninawaambieni, mwogopeni huyo.  

 

 

-

6


 

  Inajulikana kwamba shomoro watano huuzwa kwa senti kumi, au sivyo? Lakini mbele ya Mungu hasahauliki hata mmoja.  

 

 

-

7


 

  Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope, basi, ninyi mna thamani zaidi kuliko shomoro wengi!  

 

 

-

8


 

  "Nawaambieni kweli, kila mtu anayekiri hadharani kwamba yeye ni wangu, Mwana wa Mtu naye atakiri mbele ya malaika wa Mungu kwamba mtu huyo ni wake.  

 

 

-

9


 

  Lakini, mtu yeyote anayenikana mbele ya watu, naye atakanwa mbele ya malaika wa Mungu.  

 

 

-

10


 

  "Yeyote anayesema neno la kumpinga Mwana wa Mtu atasamehewa; lakini anayemkufuru Roho Mtakatifu hatasamehewa.  

 

 

-

11


 

  "Watakapowapeleka ninyi mbele ya masunagogi na mbele ya wakuu na watawala msiwe na wasiwasi juu ya jinsi mtakavyojitetea au jinsi mtakavyosema.  

 

 

-

12


 

  Kwa maana wakati huo Roho Mtakatifu atawafundisheni kile mnachopaswa kusema."  

 

 

-

13


 

  Mtu mmoja katika ule umati wa watu akamwambia, "Mwalimu, mwambie ndugu yangu tugawane urithi aliotuachia baba."  

 

 

-

14


 

  Yesu akamjibu, "Rafiki, ni nani aliyeniweka mimi mwamuzi au msuluhishi kati yenu?"  

 

 

-

15


 

  Basi, akawaambia wote, "Jihadharini na kila aina ya tamaa; maana uzima wa mtu hautegemei wingi wa vitu alivyo navyo."  

 

 

-

16


 

  Kisha akawaambia mfano: "Kulikuwa na tajiri mmoja ambaye shamba lake lilizaa mavuno mengi.  

 

 

-

17


 

  Tajiri huyo akafikiri moyoni mwake: `Nitafanyaje nami sina mahali pa kuhifadhia mavuno yangu?  

 

 

-

18


 

  Nitafanya hivi: nitabomoa ghala zangu na kujenga kubwa zaidi, na humo nitahifadhi mavuno yangu yote na mali yangu.  

 

 

-

19


 

  Hapo nitaweza kuiambia roho yangu: sasa unayo akiba ya matumizi kwa miaka na miaka. Ponda mali, ule, unywe na kufurahi.`  

 

 

-

20


 

  Lakini Mungu akamwambia: `Mpumbavu wewe; leo usiku roho yako itachukuliwa. Na vitu vile vyote ulivyojilundikia vitakuwa vya nani?"`  

 

 

-

21


 

  Yesu akamaliza kwa kusema "Ndivyo ilivyo kwa mtu anayejilundikia mali kwa ajili yake mwenyewe, lakini si tajiri mbele ya Mungu."  

 

 

-

22


 

  Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake, "Kwa sababu hiyo nawaambieni, msiwe na wasiwasi juu ya chakula mnachohitaji ili kuishi, wala juu ya mavazi mnayohitaji kwa ajili ya miili yenu.  

 

 

-

23


 

  Kwa sababu uzima ni bora kuliko chakula, na mwili ni bora kuliko mavazi.  

 

 

-

24


 

  Chukueni kwa mfano, kunguru: hawapandi, hawavuni wala hawana ghala yoyote. Hata hivyo, Mungu huwalisha. Ninyi mna thamani zaidi kuliko ndege!  

 

 

-

25


 

  Ni nani kati yenu kwa kuwa na wasiwasi anaweza kuongeza urefu wa maisha yake?  

 

 

-

26


 

  Basi, kama hamwezi kufanya jambo dogo kama hilo, kwa nini kuwa na wasiwasi juu ya yale mengine?  

 

 

-

27


 

  Angalieni maua jinsi yanavyomea. Hayafanyi kazi wala hayafumi. Hata hivyo, nawahakikishieni kwamba hata Solomoni mwenyewe na fahari zake zote hakupata kuvikwa vizuri kama ua mojawapo.  

 

 

-

28


 

  Lakini, kama Mungu hulivika vizuri jani la shambani ambalo leo liko na kesho latupwa motoni, je, hatawafanyia ninyi zaidi? Enyi watu wenye imani haba!  

 

 

-

29


 

  "Basi, msivurugike akili, mkihangaika daima juu ya mtakachokula au mtakachokunywa.  

 

 

-

30


 

  Kwa maana hayo yote ndiyo yanayohangaikiwa na watu wasiomjua Mungu. Baba yenu anajua kwamba mnahitaji vitu hivyo.  

 

 

-

31


 

  Shughulikieni kwanza Ufalme wa Mungu, na hayo yote mtapewa kwa ziada.  

 

 

-

32


 

  "Msiogope, enyi kundi dogo! Maana Baba yenu amependa kuwapeni Ufalme.  

 

 

-

33


 

  Uzeni mali yenu mkawape maskini misaada. Jifanyieni mifuko isiyochakaa, na jiwekeeni hazina mbinguni ambako haitapungua. Huko wezi hawakaribii, wala nondo hawaharibu.  

 

 

-

34


 

  Pale ilipo hazina yako, ndipo pia utakapokuwa moyo wako.  

 

 

-

35


 

  "Muwe tayari! Jifungeni mkanda kiunoni, na taa zenu ziwe zinawaka;  

 

 

-

36


 

  muwe kama watumishi wanaomngojea bwana wao arudi kutoka arusini, ili wamfungulie mara atakapobisha hodi.  

 

 

-

37


 

  Heri yao watumishi wale ambao bwana wao atakaporudi atawakuta wanakesha! Nawaambieni hakika, huyo bwana atajifunga mkanda kiunoni, atawaketisha mezani na kuwahudumia.  

 

 

-

38


 

  Heri yao watumishi hao ikiwa bwana wao atawakuta wanakesha hata ikiwa atarudi usiku wa manane au alfajiri.  

 

 

-

39


 

  Jueni kwamba, kama mwenye nyumba angejua saa ambayo mwizi atakuja, angekesha, wala hangeiacha nyumba yake ivunjwe.  

 

 

-

40


 

  Nanyi, kadhalika muwe tayari, maana Mwana wa Mtu atakuja saa msiyoitazamia."  

 

 

-

41


 

  Petro akamwambia, "Bwana, mfano huo ni kwa ajili yetu tu, au ni kwa ajili ya watu wote?"  

 

 

-

42


 

  Bwana akajibu, "Ni nani basi, mtumishi aliye mwaminifu na mwenye busara, ambaye bwana wake atamweka juu ya watumishi wake ili awape chakula wakati ufaao?  

 

 

-

43


 

  Heri yake mtumishi huyo ikiwa bwana wake atakaporudi atamkuta akifanya hivyo.  

 

 

-

44


 

  Hakika atampa madaraka juu ya mali yake yote.  

 

 

-

45


 

  Lakini, kama mtumishi huyo atafikiri moyoni mwake: na kusema: `Bwana wangu amekawia sana kurudi` halafu aanze kuwapiga watumishi wenzake, wa kiume au wa kike, na kula, kunywa na kulewa,  

 

 

-

46


 

  bwana wake atarudi siku asiyoitazamia na saa asiyoijua; atamkatilia mbali na kumweka fungu moja na wasioamini.*fb*  

 

 

-

47


 

  Mtumishi ambaye anajua matakwa ya bwana wake lakini hajiweki tayari kufanya anavyotakiwa, atapigwa sana.  

 

 

-

48


 

  Lakini yule afanyaye yanayostahili adhabu bila kujua, atapigwa kidogo. Aliyepewa vingi atatakiwa vingi; aliyekabidhiwa vingi zaidi atatakiwa kutoa vingi zaidi.  

 

 

-

49


 

  "Nimekuja kuwasha moto duniani, laiti ungekuwa umewaka tayari!  

 

 

-

50


 

  Ninao ubatizo ambao inanipasa niupokee; jinsi gani ninavyohangaika mpaka ukamilike!  

 

 

-

51


 

  Mnadhani nimekuja kuleta amani duniani? Hata kidogo; si amani bali utengano.  

 

 

-

52


 

  Na tangu sasa, jamaa ya watu watano itagawanyika; watatu dhidi ya wawili, na wawili dhidi ya watatu.  

 

 

-

53


 

  Baba atakuwa dhidi ya mwanawe, mwana dhidi ya baba yake; mama dhidi ya bintiye, binti dhidi ya mama yake; mama mkwe dhidi ya mke wa mwanawe na huyo dhidi ya mama mkwe wake."  

 

 

-

54


 

  Yesu akayaambia tena makundi ya watu, "Mnapoona mawingu yakitokea upande wa magharibi, mara mwasema: `Mvua itanyesha`, na kweli hunyesha.  

 

 

-

55


 

  Mnapoona upepo wa kusi unavuma, mwasema `Kutakuwa na hali ya joto` na ndivyo inavyokuwa.  

 

 

-

56


 

  Enyi wanafiki! Mnajua kutabiri hali ya hewa kwa kuangalia dunia na anga; kwa nini basi, hamwezi kujua maana ya nyakati hizi?  

 

 

-

57


 

  "Na kwa nini hamwezi kujiamulia wenyewe jambo jema la kufanya?  

 

 

-

58


 

  Maana kama mshtaki wako anakupeleka mahakamani, ingekuwa afadhali kwako kupatana naye mkiwa bado njiani, ili asije akakupeleka mbele ya hakimu, naye hakimu akakutoa kwa polisi, nao wakakutia ndani.  

 

 

-

59


 

  Hakika hutatoka huko nakwambia, mpaka utakapomaliza kulipa senti ya mwisho."  

 

 

-

Luke 13

 

 

 

 

HTMLBible Software - Public Domain Software by johnhurt.com

 


Other Items are Available At These Sites: